
Kanali Mstaafu wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), Abdulrahman Omar Kinana anatajwa kuwa katika orodha ya safu za viongozi mibuyu na migude kwenye misitu minene ya siasa yenye kuhimili tufani za kila aina pia Mwanasiasa anayependa kuheshimu utamaduni, utaratibu na mwenye kuishi kwa misingi ya nidhamu .
Kinana anatajwa kama zao miongoni mwa kunga zitokanazo na mazao katika medani za siasa, utawala, uongozi na aliyeshiba ujuzi toshelezi wa masuala ya diplomasia ya siasa pia anayejua mahusiano yatokanayo na historia, harakati za ukombozi na umoja wa Afrika.
Sauti yake aghalabu huwa na mvumo wa mawimbi ya busara, fikara njema na hekima zenye wito pele aamuapo kusema, kukosoa, kutetea, kukumbusha, kushauri au kuonya kutokana na tabia yake ya kufanya yote hayo kwa hali ya kujiamini akiwa na nguvu ya hoja.
Ukimya wa Mwanasiasa huyo siku zote ni kama mfano wa Simba hodari awindae nyikani au mbugani akiwa hana pupa wala kiherehere. Huyafanya yote kwa utulivu na umakini mkubwa ambao baadae haumletei majuto, athari wala taathira.
Ni Mwanasiasa wa aina yake aliyewahi kuhitajiwa na Marais (Wenyeviti) watatu awe katibu mkuu wa CCM akakataa huku akitoa madai mazito yenye msingi, nguvu ya hoja na maana.












