Tuesday, March 25, 2014

KESI YA KUSAFIRISHA TWIGA KWENDA UARABUNI YAKWAMA TENA

Moshi,

Kesi ya usafirishaji wanyama hai kwenda Uarabuni imeshindwa kuendelea kwa mara nyingine katika mahakama ya hakimu mkazi mjini Moshi huku upande wa Jamhuri ukiomba kutolewa kwa hati ya kukamatwa kwa mshtakiwa wa kwanza Kamran Ahmed ambaye hakufika mahakamani. 

Ombi la kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo limetolewa na mawakili wa Jamhuri, Evatha Mushin na Joseph Maugo baada ya mshtakiwa huyo pamoja na wakili wake Edmundi Ngemela kutofika mahakamani bila maelezo yoyote. 


Mbele ya hakimu mkazi wa mahakama hiyo Simon Kobelo mawakili hao walidai mshtakiwa huyo hafiki mahakamani hapo kwa makusudi na kutaka awasilishe vyeti vya kupata matibabu hospitalini ambapo Feb. 26 mwaka huu kupitia kwa wakili wake Ngemela aliomba kuahirishwa kwa kesi hiyo kutokana na kupanda kwa sukari yake. 

Mawakili hao waliiomba mahakama kukamatwa kwa mshtakiwa huyo ambaye amekuwa akiisababishia hasara upande wa jamhuri kutokana na kuleta mashahidi na kuwarejesha bila ya kutoa ushahidi wao mahakamani hapo. 

Kesi hiyo ambayo ilifika mahakamani hapo kwa ajili ya shahidi wa 22 kutoa ushahidi wake ililazimika kusubiriwa kwa zaidi ya masaa sita hadi ilipoahirishwa katika mahakama ya ndani(Chamber Court) itaendelea tena leo(MACHI 25) mwaka huu. 

Hata hivyo pamoja na washitakiwa wengine watatu katika kesi hiyo Hawa mang'unyuka, Martin Kimath na Michael Mrutu wanashitakiwa kwa tuhuma za kusafirisha ndege na wanyama hao wakiwemo twiga wane wanaogharimu dola za kimarekani zaidi ya 113, 715 mnamo Novemba 26 2010. 

Katika kesi hiyo inayofuatiliwa na mamilioni ya watanzania, shahidi wa 20, Robert Nyanda alieleza mahakama alivyomtambua mshtakiwa wa kwanza(Ahmed)  siku ya tukio. 

Shahidi huyo alidai siku ya tukio alishiriki katika uandaaji wa vifaa kwa ajili ya upakiaji wa mizigo mizito katika ndege ikiwa ni maelekezo ya bosi wake Rosemery Israel ambapo pia alishuhudia gari aina ya Fuso likiwa limepakia maboksi yenye wanyama hao. 


Kwa upande wake,shahidi wa 21 katika kesi hiyo,Rewald Amani aliyekuwa meneja muongozaji wa ndege katika uwanja wa Kia,aliieleza mahakama kuwa ndege hiyo ilitua nchini Novemba 24, 2010  katika kiwanja hicho na kuondoka Novemba 26, 2010 ikiwa salama kuelekea Doha Qatar.


No comments:

Post a Comment