Thursday, June 07, 2012

MARANDA AFUNGA USHAHIDI KESI YA EPA



MSHTAKIWA na shahidi wa pili katika kesi ya wizi wa sh. bilioni 3.3 kutoka kwa  Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT),  kada wa CCM, Rajabu Maranda amefunga ushahidi wake katika kesiinayomkabili na wenzake watano.

Hatua hiyo ilifikiwa mara baada ya Bw. Maranda kumaliza kutoa ushahidi wake mbele ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaama, jana ambapo alikana tuhuma zote zinazomkabili na kuiomba mahakama kutupilia mbali shauri hilo.

Katika kesi hiyo Bw. Maranda,binamu yake Bw.Farijala Hussein, Bw.Ajay Somani na wafanyakazi watatu wa  benki hiyo wanadaiwa kufanya njama na kuiba fedha hizo.

Pia washtakiwa hao, Bw.Maranda Bw.Hussein, Ajay na wafanyakazi wa BoT,  Imani Mwaposya, Ester Komu na Sophia Kalika  kwa pamoja wanadaiwa kuiba sh. bilioni 3.3  za EPA kutoka kwenye benki hiyo baada kudanganya kuwa kampuni yao ya Mibale Farm imepewa deni na kampuni ya Textile Mills Ltd ya nchini India na kujipatia kiasi hicho.

Mahakama imehairisha kesi hiyo hadi leo ambapo itasilizwa tena na jopo la majaji wanaoendesha kesi hiyo.

Washtakiwa Farijala Hussein, Rajabu Maranda na Ajay Somani wanadaiwa kuwa kati ya Januari 18 na Novemba 3, 2005, kinyume na kifungu namba 384 cha kanuni ya adhabu sura ya 16 ya sheria, walikula njama ya wizi wa fedha kutoka BoT.

Pia wanadaiwa kughushi hati ya usajili yenye namba 46218 na kuonesha kuwa zimesainiwa  na kutolewa na Msajili wa Biashara kwa Kampuni ya Mibale Farm wakati si kweli.



No comments:

Post a Comment