Wednesday, March 07, 2018

WAJIBU WA WACHIMBAJI WADOGO NI KUFUATA MAELEKEZO NA KULIPA KODI KWA UAMINIFU


PICHANI : Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko akiwaeleza wachimbaji wadogo wa madini ya dhahabu katika Kijiji cha Bululu, kilichopo katika Kata ya Nyamtukuza Wilaya ya Nyang'wale Mkoani Geita juu ya umuhimu wa kufuata taratibu na sheria katika uchimbaji, Jana 6 Machi 2018. Picha Zote Na Mathias Canal-Wazo Huru Blog

Na Mathias Canal, Geita

Serikali imesema kuwa imedhamiria kuwanufaisha wananchi wake kupitia rasilimali za nchi hususani sekta ya Madini hivyo jukumu la Wachimbaji hao ni kufuata maelekezo ya serikali ikiwemo taratibu na sheria katika uchimbaji.

Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko ametoa rai hiyo Jana 6 Machi 2018 wakati akizungumza na wachimhaji wadogo katika Kijiji cha Bululu, kilichopo katika Kata ya Nyamtukuza Wilaya ya Nyang'wale Mkoani Geita.

Alisema kuwa Serikali tayari imetenga maeneo maalumu kwa wachimbaji wadogo katika mkoa wa Geita na maeneo mengi nchini huku akisisitiza kuwa kuna leseni za utafiti na uchimbaji mdogo 20 ambazo zinaisha muda wake 30 Machi mwaka huu katika Wilaya ya Nyang'wale hivyo wananchi wanapaswa kuwa wavumilivu katika kipindi hicho kwani serikali inatazama namna ya kuwapatia wachimbaji wadogo baadhi ya maeneo hayo.

Mhe Biteko alisisitiza hayo wakati akijibu maswali ya wachimbaji wadogo waliohudhuria mkutano wa hadhara na kuiomba serikali kuwapatia maeneo rasmi kwa ajili ya uchimbaji kwani katika kipindi kirefu wamekuwa wakizuiwa kuchimba katika maeneo mbalimbali ambayo yana leseni za uchimbaji.

Alisema kuwa serikali itatoa leseni kwa ajili ya maeneo ya uchimbaji lakini haitatoa leseni hizo kwa mtu mmoja mmoja badala yake amewasihi wachimbaji hao kuanzisha vikundi ili kupatiwa leseni hizo.

Mhe Biteko pia alimuagiza Mkuu wa Wilaya ya Nyang'wwale Mkoani Geita Mhe Hamim Gwiyama kuitisha kikao ndani ya wiki moja kwa kuwaalika wananchi wote wenyewe vikundi ili kuwaelekeza namna bora ya kufanya kazi za uchimbaji kwa kufuata taratibu na sheria.

Aidha, amewataka Wachimbaji hao Mara baada ya kupewa maeneo ya uchimbaji kuwa waaminifu kwa serikali yao kwa kulipa kodi ili kuiwezesha serikali kuboresha huduma za maendeleo ikiwemo sekta ya Afya, elimu na miundombinu.


Wachimbaji wadogo wa madini ya dhahabu katika Kijiji cha Bululu, kilichopo katika Kata ya Nyamtukuza wakimsikiliza kwa makini Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko wakati akiwa katika ziara ya kikazi Wilaya ya Nyang'wale Mkoani Geita, Jana 6 Machi 2018.


Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko akiwaeleza akisisitiza jambo wakati aliokuwa akihutubia wananchi wakati akiwa katika ziara ya kikazi Wilaya ya Nyang'wale Mkoani Geita, Jana 6 Machi 2018.


Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko (Kulia) na Mbunge wa Jimbo la Nyang'wale Mhe Hussein Nassor Amari Kasu (Kulia) wakisikiliza kero za wananchi wakati wa ziara ya kikazi Wilaa ya Nyang'wale Mkoani Geita, Jana 6 Machi 2018.




No comments:

Post a Comment