Monday, February 12, 2018

BREAKING NEWS: AJALI MBAYA YAUA 5 NA KUJERUHI, NI BASI LA AJ NA HIACE

Na Yusuph Mussa, Korogwe

WATU watano wamepoteza maisha na wengine sita kujeruhiwa vibaya baada ya basi la Kampuni ya AJ lenye namba T 497 BJB linalofanya safari zake kutoka Lushoto kwenda Dar es Salaam kugongana uso kwa uso na hiace maeneo ya Kata ya Kabuku, Wilaya ya Handeni mkoani Tanga( PICHANI).

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mchana wa leo Februari 12, 2018, Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga Leonce Rwegasira alisema ajali hiyo imetokea leo saa tano asubuhi.

Rwegasira alisema ajali hiyo imetokea kati ya basi hilo lililokuwa linatoka Lushoto kwenda Dar es Salaam na basi dogo aina ya hiace lenye namba T 591 AKE ambalo linafanya safari zake kati ya Njia Panda ya Segera na Mkata wilayani Handeni na ilikuwa inakwenda Mkata.

Alisema chanzo cha ajali hiyo ni madereva kushindwa kufuata sheria za barabarani, ambapo magari hayo yamegongana uso kwa uso na kusababisha vifo na majeruhi.

"Ajali hii iliyotokea kwenye saa tano, chanzo chake ni madereva kushindwa kufuata sheria za barabarani, ambapo ndipo madereva wakagongana uso kwa uso. Tumeshindwa kuwatambua madereva wa magari hayo kwa vile inadhaniwa dereva wa hiace ni miongoni mwa waliopoteza maisha.

"Lakini dereva wa basi kubwa tuna uhakika yupo hai, lakini ni majeruhi, hivyo tunawaachia kwanza madaktari wa Hospitali ya Magunga, Korogwe wampe matibabu, ndiyo tumjue jina na kupata maelezo mengine.

Mwandishi wa habari hizi ambaye yupo mjini Korogwe, alishuhudia magari manne, ambapo mawili ya polisi, yakiwa yamebeba maiti na majeruhi yakielekea Hospitali ya Wilaya ya Korogwe, Magunga.

2 comments:

  1. Mola awape nafuu majeruhi na marehemu wapumzike kwa Amani tijiandae tupo safarin dunian sio kwetu. By Mpwapwa habariblogspot

    ReplyDelete