Monday, September 18, 2017

UONGOZI WA SHIRIKA LA POSTA TANZANIA WAKUTANA NA WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO


Baadhi ya Maofisa wa Wizara ya Fedha na Mipango wakifuatilia kwa makini, mazungumzo kati ya Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Phillip Mpango na Uongozi wa Shirika la Posta Tanzania (TPC), jijini Dar es Salaam leo. Katikati ni Mchumi Mkuu wa wizara, Dionisia Mjema.(Picha zote na Bw. Elia Madulesi)


Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Phillip Mpango akiwa na Kamishina wa Sera, Bw. Mgonya Benedicto wasikiliza taarifa za Shirika la Posta kupitia kwa Postamasta Mkuu Bw. Deo Kwiyukwa (hayuko pichani), wakati wa ziara hiyo leo.


18 Septemba, 2017

UONGOZI wa Shirika la Posta Tanzania (TPC), leo umefanya ziara Wizara ya Fedha na Mipango na kufanya mazungumzo na Waziri wa wizara hiyo, Dkt. Philip Mpango, Ofisini kwake jijini Dar es Salaam.

Ujumbe huo wa Shirika la Posta uliongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika, Kanal Mstaafu Dkt. Harun Kondo, akiwa na Kaimu Postamasta Mkuu Bw. Deogratius Kwiyukwa,Kaimu Meneja Mkuu wa Rasilimali za shirika, Bw. Macrice Mbodo na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano, Bw. Elia Madulesi.

Katika mazungumzo hayo, ujumbe kutoka Shirika la Posta ulimweleza Waziri hali halisi ya Shirika, zikiwemo changamoto , mafanikio na maendeleo ambayo shirika limeyapata tangu lilipoanzishwa mwaka 1994 baada ya kutenganishwa na Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL) na Benki ya Posta ambao kwa sasa ni taasisi zinazojitegemea kama ilivyo Shirika la Posta.
Mwenyekiti alieleza juu ya hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Shirika katika kulifanyia mabadiliko makubwa ya kimuundo na kiutendaji ili liweze kukabiliana na changomoto za ushindani wa huduma na biashara kwa jumla. Pamoja na mambo mengine Mwenyekiti wa Bodi, Dkt. Harun Kondo, alimwomba Waziri Mpango, alisaidie Shirika katika kutatua changamoto mbali mbali.

Baadhi ya changamoto alizozitaja katika mazungumzo hayo ni pamoja na;

Shirika la Posta kuwekwa kwenye orodha ya Mashirika yanayotarajiwa kurekebishwa au kubinafsishwa hatua iliyolidhoofisha Shirika. pamoja kikwazo hicho shirika la posta linabeba mzigo mkubwa wa kuwalipa watumishi wake mishahara na marupurupu yao bila kuitegemea Serikali ikizingatiwa kwamba Shirika halikupewa mtaji na haliruhisiwa kukopa kwa ajili ya kujiendesha.

Mwenyekiti wa Bodi alimkumbusha Waziri kuwa Shirika la Posta ni mali ya Serikali kwa asilimia mia moja (100%) na sheria namba 19 ya mwaka 1993 iliyoanzisha Shirika la Posta inatamka wazi kuwa Serikali kupitia Waziri wa Fedha atakaa na Waziri mwemye dhamana ya Posta ili kubaini mtaji utakaowezesha Shirika kujiendesha, hadi sasa mtaji huo haujaweza kutolewa ili kuliwezesha Shirika kujiendesha.

Pia Mwenyekiti amemwomba Waziri ili Shirika lirejeshewe fedha kiasi cha shilingi 3,977,000,000/= ambazo Shirika lilizitumia kulipa Pensheni ya wastaafu wa lililokuwa Shirika la Posta na Simu la Jumuia ya Afrika Mashariki.

Vilevile alimuomba Waziri kuhamisha jukumu la kuwalipa wastaafu hao kwenye Mifuko ya hifadhi ya jamii.

Serikali iangalie uwezekano wa kuchukua mzigo wa riba na tozo (Interest and Penalty) na malimbikizo ya kodi ya shilingi 29,000,833,757/= ambayo kati ya hizo, tozo na riba ni shilingi 22,013 701,414.28.

Mwenyekiti alimweleza Mheshimiwa Waziri kuwa haya yote yakifanyika kwa wakati Shirika litaweza kujiendesha kwa faida na kutoa gawio kwa mwenye mali (Serikali) kama ilivyokusudiwa.

Pia alieleza kuwa kwa sasa Shirika linafanya mabadiliko makubwa ya kimfumo na ya kimuundo ambapo linahitaji fedha kwa ajili ya kuboresha huduma zake, kuanzisha miradi mipya na kuimarisha zile zilizoko.

Mwisho, Waziri Dkt. Mpango aliahidi kuyafanyia kazi maombi hayo kwa karibu na kuangalia namna ya kutatua changamoto hizo kwa kushirikiana na Wizara inayosimamia Shirika la Posta liweze kutoa huduma bora katika vituo yake, kujiendesha kwa faida na hatimaye kuweza kutoa gawio kwa Serikali.



Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Phillip Mpango akitoa maelekezo kwa Mkurugenzi wa Sera Bw. Mgonya Benedicto, wakati alipokuwa anazungumza na uongozi wa Shirika la Posta, ulipomtembelea ofisini kwake leo jijini Dar es Salaam.



Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Posta Tanzania (TPC), Kanali mstaafu, Dkt. Harun Kondo (kushoto), akimweleza jambo Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango wakati Uongozi wa shirika hilo, ulipomtembelea ofisini kwake jijini Dar es Salaam leo.






Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Posta Tanzania (TPC), Kanali mstaafu, Dkt. Harun Kondo (kushoto), akimweleza jambo Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango wakati Uongozi wa shirika hilo, ulipomtembelea ofisini kwake jijini Dar es Salaam leo. Kushoto ni Kaimu Postamasta Mkuu, Bw. Deo Kwiyukwa na kulia ni Mkurgenzi wa Sera wa wizara hiyo, Bw. Mgonya Benedicto.



Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Posta Tanzania (TPC), Kanali mstaafu, Dkt. Harun Kondo (kushoto), akimweleza jambo Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango wakati Uongozi wa shirika hilo, ulipomtembelea ofisini kwake jijini Dar es Salaam leo. Kushoto ni Kaimu Postamasta Mkuu, Bw. Deo Kwiyukwa.



Picha ya pamoja ya uongozi wa Shirika la Posta wakiwa na Waziri wa Fedha na Mipango Dr. Philip Mpango(wa pili kushoto) baada ya ujumbe huo kumtembelea ofisini kwake Jijini Dar es Salaam.



Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Posta Tanzania (TPC), Kanali mstaafu, Dkt. Harun Kondo (wa pili kulia), akimshukuru Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, mara baada uongozi huo, kumtembelea ofisini kwake na kufanya naye mazungumzo, jijini Dar es Salaam leo. Kushoto ni Kaimu Postamasta Mkuu, Bw. Deo Kwiyukwa na kulia ni Meneja Mkuu Rasilimali za shirika, Bw. Macrice Mbodo.






No comments:

Post a Comment