MGOMBEA wa ubunge wa Jimbo
la Ubungo kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt Didas Masaburi, amekana
kuhusika na uuzwaji wa mali za Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA) na kutupa
mzigo huo kwa mgombea wa urais kupitia CHADEMA, Edward Lowassa.
Dkt. Masaburi amedai
kushangazwa na kauli zinazotolewa na wapinzani wake hasa wa vyama vya upinzani
wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), wakimtuhumu kuhusika kwake na
uuzwaji wa mali za UDA wakati si kweli.
Akizungumza katika kampeni
zake zilizofanyika Kata ya Makuburi juzi, Dkt. Masaburi alidai Lowassa akiwa
Waziri Mkuu ndiye aliyehusika na uuzwaji wa UDA kwani alisimamia kwa kina
kuhakikisha hilo linafanikiwa.
“Kipindi mimi nilipokuwa meya
(wa Dar es Salaam) nilikuta tayari aliyekuwa waziri mkuu kipindi hicho Edward
Lowassa amesaini mikataba ya uuzaji wa hisa za UDA, sasa nani fisadi hapa?”
Alihoji.
Dkt. Masaburi alidai,
wakati akiwa meya aliikuta Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ikiwa inamiliki
mali nyingi, lakini wajanja walikuwa wakifaidika binafsi ndipo alipoamua kupitia mikataba yote na kubaini ubadhirifu
huo wa UDA.
“UDA iliuzwa kwa kampuni
ya Simon Group kwa Sh milioni 285, lakini nilipohoi kuhusu hizo fedha
nikaambiwa zipo Sh milioni 85 na Sh milioni 200 hazijulikani zilipo, niliamua
kuivunja bodi ya shirika hilo na kuwasimamisha kazi baadhi ya watendaji ili
kupisha uchunguzi,” alisema.
Alifafanua kuwa, wakati
hisa za UDA zinauzwa mwaka 2008 hakuwa meya wa Jiji la Dar es Salaam na
alipoingia ndipo alipokuta uozo mwingi na kuanza kusafisha baadhi ya mambo.
“Kumekuwa na wimbi kubwa
la wagombea wanaotumia vibaya majina ya vyama au wagombea wengine kuwachafua
ikiwa ni moja ya sera zao wanapopanda
majukwaani, wanasahau kuwa miongoni mwa watu wanaowasema ni viongozi wao wenyewe,”
alisema.
Dkt. Masaburi alisema, endapo
atachaguliwa kuliongoza jimbo hilo atahakikisha anashirikiana na Serikali katika
kuboresha miundombinu mbalimbali ikiwemo
barabara za ndani ya mitaa kwa
kiwango cha lami, kuhakikisha maji safi na salama yanapatikana na kuongeza
ajira kwa vijana kupitia mradi wa mabasi
yaendayo kasi (DART) na miradi mingine.
Alisema moja kati
vipaumbele vyake ni kuboresha elimu na vituo vya afya, kurekebisha mifumo ya
majitaka pamoja na kuwatengea wanawake na watu wa makundi maalumu mfuko
utakaowawezesha kukopa.
No comments:
Post a Comment