Saturday, April 12, 2014

ZITTO AWAJIBU RAIS KIKWETE NA JAJI WARIOBA, SOMA HAPA. . .


Majibu kwa Malalamiko ya Warioba na Hofu za Kikwete
Na Zitto Kabwe

TANGU kuanza kwa Bunge Maalumu la Katiba (BMK), nimekuwa mkimya kuliko nilivyozoeleka katika maisha yangu ya kisiasa. Watu wengi wamekuwa wakiniuliza maswali kuhusu nini msimamo wangu katika masuala anuai yanayojadiliwa ndani ya Bunge.

Hata hivyo, kuliko jambo lingine lolote, ukimya wangu ulitokana na uzito wenyewe wa jambo ambalo BMK unatakiwa kulifanya. Inapaswa kufanya utafiti mkubwa kabla ya kuzungumza maana haya tunayoyafanya sasa yatakuja kusomwa katika vitabu vya historia miaka mingi baada ya sisi sote kuondoka katika ulimwengu huu.
Bila shaka, uamuzi mkubwa zaidi ambao BMK linatarajiwa kuufanya ni kuhusu aina ipi ya ushirika au mahusiano ambao nchi yetu sasa itaamua kuufuata kupitia Katiba Mpya tunayotaka kuipitia.
Ni kuhusu idadi ya serikali tutakazokuwa nazo na uhusiano utakaokuwepo. Serikali mbili au tatu. Tume ya Jaji Joseph Warioba ilipendekeza muundo wa serikali tatu lakini inaonekana Rais Jakaya Kikwete na serikali yake ya CCM wanapendelea kuendelea na mfumo wa sasa wa serikali mbili.
Jambo moja ambalo nimejifunza wakati nikifanya utafiti na kufuatilia mijadala mbalimbali inayoendelea kuhusu suala hili ni kwamba Watanzania wengi wanapenda Muungano wetu uendelee. Niseme mapema kwamba Watanzania hatupaswi kuiga isipokuwa kujifunza kwa nchi nyingine. Hivyo muundo gani unafaa ni uamuzi wetu wenyewe. Hata hivyo uamuzi huo ni lazima ujibu vigezo fulani fulani.
Vigezo vikubwa ni viwili; Je, Muundo tunaoutaka utajibu kero (malalamiko) za Muungano wa sasa? Je, Muundo tunaoutaka utajibu hofu za Muungano kuvunjika. Muundo utakaojibu hofu hizo ndio utakaotufaa. Suala la serikali ngapi zinatakiwa ni suala linalokuja baadaye baada ya kujibu hoja hizo za msingi.

Kwa sasa, bado kuna utata iwapo Tanzania ni Shirikisho (Federation) au ni Muungano (Union). Katika vikao vya Kamati za BMK vinavyoendelea sasa, jambo hili limezua mjadala mkubwa ambapo baadhi ya wajumbe wanapendekeza kuwa neno Shirikisho litoke kwenye Sura ya Kwanza ya Rasimu ya Katiba na wengine wakipendekeza libakie au hata kuweka wazi kabisa kuwa Tanzania ni Jamhuri ya Shirikisho la Tanganyika na Zanzibar.
Ni vema, kama mtu mwenye mapenzi mema na Taifa lake, nikatumia fursa hii kuzieleza dhana hizi za muundo ili zieleweke vizuri na watumiaji waweze kuzitumia kwa usahihi. Kwa ufupi tutazame maana ya kila dhana na mifano mbalimbali duniani. Tutatazama dhana tatu kuu - Muungano (Union), Shirikisho (Federation) na Jumuiya (Confederation/Community).

Muungano
Katika mfumo huu, Nchi kuungana kuunda Taifa moja, Dola moja ndani ya Nchi moja. Serikali za Washirika huachia sehemu kubwa ya madaraka yao kwa Serikali ya Muungano. Mara nyingi muundo huu hupelekea kuwapo kwa Serikali moja yenye nguvu (ya Muungano) na kama Washirika wanabakia na serikali zao, basi hubakia na mambo machache sana. Faida ya Muundo huu iko kwenye uimara wake na si rahisi kuvunjika.
Hasara za muundo huu ni athari ya moja ya nchi, hasa kama ni ndogo, kumezwa na Mshirika mkubwa. Hapa Afrika, Nchi ya Afrika ya Kusini inafuata muundo huu wa Muugano ambapo Serikali ya Muungano ina nguvu na mamlaka mengi kuliko zile za Majimbo yanayounda Jamhuri ya Afrika ya Kusini. Huko Asia mfano mzuri ni India ambapo japo muundo wake unatoa nguvu kubwa kwa Majimbo kujitawala, Serikali ya Muungano (Union Government) ina nguvu kubwa zinazoondoa sifa ya kuitwa Shirikisho.
Si lazima 'Union' kuwa na Serikali moja (Unitary State) isipokuwa mazingira ya nchi husika ndio yanaweza kuamua. Mfano mzuri hapa ni ule wa Afrika ya Kusini ambayo ni 'unitary state' yenye Serikali 10, tisa za Majimbo na Moja ya Muungano.

Shirikisho
Katika muundo huu, serikali za washirika hukasimu sehemu ndogo ya madaraka yake kwa Serikali ya Muungano. Mambo ya kidola (sovereign functions) hufanywa na Serikali ya Shirikisho na Serikali za Washirika kubakia na mambo yake yenyewe.
Faida kubwa ya muundo huu ni kuondoa hofu ya mkubwa kummeza mdogo na ule uhuru wa kujiamulia mambo mengi. Hasara ya muundo huu ni kujengwa kwa utaifa au hisia za utaifa za Washirika ambazo hatimaye hupelekea Shirikisho kuvunjika. Hapa Afrika mfano mzuri wa Shirikisho ni nchi ya Ethiopia ambapo Majimbo yake yanao uwezo hata wa kujitoa katika Shirikisho kikatiba.
Eritrea ilitumia fursa hii na kujitoa kuwa sehemu ya Ethiopia mara baada ya mapinduzi yaliyomtoa Mengistu Haile Mariam. Ujerumani pia ni Shirikisho.

Jumuiya

Katika muundo huu kila Mshirika anakuwa na uhuru wa mambo yake yote isipokuwa tu kunakuwa na mambo ya uratibu wa pamoja. Aina hii ya Muundo ndio unapaswa kwa kinachoitwa Muungano wa Mkataba.
Faida kubwa ya muundo huu ni kwamba hakuna kubanana na pale kunapotokea hofu Mshirika hujitoa. Mfano mzuri ni Uswisi na Jumuiya ya Ulaya. Hata Jumuiya ya Afrika Mashariki pia inaitwa ni Muungano wa Mkataba.

Muundo gani Tanzania?
Tanzania kuwa Shirikisho au Muungano ni mjadala ambao utaendelea kuwapo licha ya kuamua kuchagua muundo mmoja wapo. Wakati wa kuandika Katiba ya India mwaka 1947 ubishani huu ulikuwa mkubwa sana pia.
Katiba ya India imegawanya mamlaka katika sehemu tatu - Mambo ya Muungano, Mambo ya Washirika na Mambo ya Pamoja (concurrent). Wajumbe wa Bunge la Katiba la India wanaotaka Shirikisho walipinga muundo huo na kukataa 'Washirika kuwa ombaomba kwa Serikali ya Muungano'.
Hata hivyo ubishi huo ulimalizwa na Mwanasheria mahiri wa India, BM Ambedkar, kwa kusema 'tunataka Serikali imara ya Muungano na yenye nguvu iwezekanvyo' na alifunga mjadala kwa kusema 'Muungano wa Washirika unatakiwa zaidi kuliko Shirikisho la Washirika'.

Tanzania inaweza kuwa na Muundo wa Muungano wenye Serikali tatu ama Muundo wa Shirikisho wenye Serikali mbili, ama kinyume chake. Idadi ya Serikali haina uhusiano wowote na ama tunaitwa Shirikisho au Muungano. Mifano miwili hapo juu ituongoze, India ni Muungano unaitwa Shirikisho na Afrika Kusini ni Shirikisho linaloitwa Muungano.
Muungano wa Serikali 3 na sio Shirikisho la Serikali 3 ndio mapendekezo yangu. Muungano (Union) wa Washirika ni bora, imara na endelevu zaidi kwa mazingira ya Afrika kuliko Shirikisho (Federation) la Washirika.

Mapendekezo yangu mahususi yaliyowasilishwa kwenye kamati namba 12 ya BMK ni kama ilivyo hapa chini.

SURA YA KWANZA
SEHEMU YA KWANZA
1(1) Irekebishwe na kuandikwa upya na isomeke

Tanzania ni Nchi Moja na ni Jamhuri ya Muungano yenye mamlaka kamili
ambayo imetokana na Muungano wa Nchi za Jamhuri ya Tanganyika na
Jamhuri ya Watu wa Zanzibar ambazo kabla ya Hati ya Makubaliano ya
Muungano ya Mwaka 1964, zilikuwa nchi huru.

1(2) neno Shirikisho lifutwe na kuongeza maneno ....Nchi ya.... baada
ya neno 'ni' na kabla ya neno 'kidemokrasia'

Ongeza ibara ya mpya ya 3 itakayosomeka

3(1) Shughuli zote za Mamlaka ya Nchi katika Jamhuri ya Muungano
zitatekelezwa na kudhibitiwa na vyombo vitatu vyenye mamlaka ya
Utendaji, vyombo vitatu vyenye mamlaka ya kutekeleza utoaji haki, na
pia vyombo vitatu vyenye madaraka ya kutunga sheria na kusimamia
utekelezaji wa shughuli za umma

3(2) Vyombo vyenye Mamlaka ya Utendaji vitakuwa ni Serikali ya Jamhuri
ya Muungano, Serikali ya Zanzibar na Serikali ya Tanganyika; vyombo
vyenye Mamlaka ya kutekeleza utoaji haki vitakuwa ni mahakama ya Juu
ya Jamhuri ya Muungano, Mahakama ya Tanganyika na Mahakama ya Zanzibar na vyombo vyenye Mamlaka ya ya kutunga sheria na kusimamia utekelezaji wa shughuli za umma vitakuwa ni Bunge la Jamhuri ya Muungano, Baraza la Wawakilishi la Tanganyika na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar.

3(3) Kwa ajili ya utekelezaji bora wa shughuli za umma katika Jamhuri
ya Muungano, na kwa ajili ya mgawanyo wa madaraka juu ya shughuli hizo
baina ya vyombo vilivyotajwa katika ibara hii, kutakuwa na mambo ya
Muungano kama yalivyoorodheshwa katika Nyongeza ya Kwanza ya Katibahii, kutakuwa na mambo ya uratibu wa pamoja na kutakuwa na mambo yasiyo ya Muungano ambayo ni mambo mengine yote yasiyo mambo ya Muungano na yasiyo ya uratibu wa pamoja.

3(4) Kila chombo kilichotajwa katika ibara hii kitaundwa na kutekeleza
majukumu yake na Katiba za Serikali za Washirika na kwa kufuata
masharti ya katiba hii.

3(5) Kwa ajili ya utekelezaji bora wa shughuli za Serikali ya Jamhuri
ya Muungano au Serikali ya Tanganyika au Serikali ya Zanzibar Bunge
laweza kuigawa Jamhuri ya Muungano katika Mikoa kwa mujibu wa Sheria
iliyotungwa na Bunge; Isipokuwa kwamba Bunge litapata kwanza Azimio la Baraza la Wawakilishi la Tanganyika kwa mikoa ya Tanganyika au Baraza la Wawakilishi Zanzibar kwa mikoa ya Zanzibar.

SABABU ZA MAREKEBISHO YANAYOPENDEKEZWA.
Rasimu ya Katiba imetangaza tu kuwa 'Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
(JMT) ni Nchi' na kuacha 'ambiguity' ya kwamba Tanzania ni nchi ngapi.
Katiba ya sasa imetamka bayana kuwa 'Tanzania ni Nchi Moja'.
Rasimupia imetamka kwamba JMT inatokana na 'muungano wa nchi mbili'. Hivyo basi ni vema kuweka wazi kabisa kuwa Nchi hizi mbili zimeunda nchi
moja. Hii itaepusha migongano ya siku za usoni kuhusu tafsiri ya
Katiba na Mamlaka za Nchi. Ifahamike wazi kuwa idadi ya Serikali haina
uhusiano na uundaji wa nchi moja.

Rasimu imetangaza kuwa Tanzania ni Shirikisho ingawa bado imetamka
'Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (United Republic of Tanzania). Dhana
za 'Union' na 'Federation' ni dhana mbili tofauti katika miungano.
Idadi ya Serikali haina mahusiano ya moja kwa moja na aina ya Muungano
kama ni 'Union' au ni 'Shirikisho'. Kwa mazingira ya Nchi za Kiafrika
ni salama zaidi kuwa na 'Union' kuliko Shirikisho.

Rasimu imeweka sura ya Kwanza bila kutaja vyombo vya Jamhuri ya
Muungano. Ni vema ili kuondoa 'ambiguity' vyombo vya Jamhuri ya
Muungano kutajwa kinagaubaga katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano
katika sura ya 'uundwaji wa nchi'. Mapendekezo ya ibara mpya za sehemu
ya kwanza ya sura ya kwanza yanazingatia tahadhari hiyo. Katika kutaja
vyombo mapendekezo haya yanaonyesha dhahiri kuwa ugawaji wa Nchi
katika Mikoa inakuwa ni mamlaka ya Bunge.
Serikali za Washirika zaweza kuwa na mamlaka ya Serikali za Mitaa. Mikoa inapaswa kuwa mamlaka ya Bunge la Muungano kwa sababu yaweza pia kutumika katika kupata Wabunge wa Muungano lakini pia itasaidia kuondoa tabia ya kugawa mikoa hovyohovyo.
Kimsingi ilipaswa Mikoa yote ya Nchi itajwe ndani ya Katiba kuongezeka au kupunguka kwake kutokane na maamuzi maalumu ya Bunge hata ikibidi iwe kwa theluthi mbili.

SURA YA SITA
Ibara ya 60(1) maneno shirikisho yafutwe na kubaki uwepo wa Serikali 3.

60(3) isomeke

Muundo, madaraka na mambo mengine ya kiutendaji yahusuyo Serikali ya
Tanganyika, na Serikali ya Zanzibar yataanishwa katika Katiba za
Washirika na kwa kuzingatia masharti ya Katiba hii.

Ibara ya 63 iitwe 63(1)

Iongezwe 63(2)

Kwa ajili ya uratibu bora wa shughuli za Mamlaka za Nchi na kwa ajili
ya kuhakikisha ufanisi na weledi katika uendeshaji bora wa Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mgawanyo wa madaraka, Serikali ya Jamhuri ya Muungano itakuwa na mamlaka ya uratibu juu ya mambo ya
uratibu kama yalivyoorodheshwa katka nyongeza ya pili ya Katiba hii.

64(1) maneno nchi washirika yaondoke na kubakia neno Washirika au
Washirika wa Muungano.

64(5) isomeke

Serikali za Washirika zitakuwa na hadhi na haki sawa ndani ya Jamhuri
ya Muungano na zitatekeleza majukumu yao kwa mambo yote yasiyo ya
Muungano katika mamlaka za Serikali za Washirika kwa mujibu wa
masharti yatakayowekwa na Katiba za Serikali za Washirika kwa
kuzingatia masharti ya Katiba hii.

65 maeneo yote yenye maneno Nchi Washirika yafutwe na kuandikwa
Washirika wa Muungano

67 ifutwe yote

69 maneno Nchi yafutwe ....katiba za Washirika.......

69 (2) maneno Viongozi wakuu yafutwe na kuandikwa ' Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na Wakuu wa Serikali za Washirika watakuwa ni
Viongozi Wakuu wa Nchi'

69(3) isomeke

Viongozi wanaohusika na masharti ya ibara hii ni

(a) Rais wa Jamhuri ya Muungano
(b) Mkuu wa Serikali ya Tanganyika ambaye pia atakuwa Makamu wa Rais
wa Jamhuri ya Muungano
(c) Mkuu wa Serikali ya Zanzibar ambaye pia atakuwa Makamu wa Rais wa
Jamhuri ya Muungano.

Ongeza ibara ya 70

(1) Mkuu wa Nchi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye ataitwa
Rais atapatikana kwa kuchaguliwa kwa kura na wananchi wote wa Jamhuri
ya Muungano kwa Mujibu wa masharti ya Katiba hii. Rais atakuwa pia
Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano.

(2) Wakuu wa Serikali za Washirika watapatikana kutoka kwenye Mabaraza
ya Wawakilishi ya Washirika kutoka Chama cha siasa chenye wawakilishi
wengi kwa mujibu wa masharti yatakayowekwa na Katiba za Washirika na
kwa kuzingatia masharti ya Katiba hii.

SABABU ZA MAPENDEKEZO
Lengo ni kuhakikisha kuwa Jamhuri ya Muungano inabakia ni nchi moja
yenye serikali 3 zenye mamlaka na madaraka yake yaliyofafanuliwa na
katiba.
Kwa kuwa tunaamua kuwa na Nchi moja basi Serikali zinazoundwa
zitakuwa ni Serikali Washirika na sio nchi Washirika tena kama rasimu
inavyoita.
Kuweka wazi kuwa ni kiongozi mmoja tu wa Serikali ndio
atachaguiwa na wananchi wote wa Jamhuri ya Muungano naye ni Rais -
Mkuu wa Nchi na Amiri Jeshi Mkuu wa majeshi ya Ulinzi na usalama.
Majina ya Wakuu wa Serikali za Washrika yatatolewa na kwa mujibu wa
Katiba zao na hivyo hakuna sababu kwa Katiba ya Muungano kuunda majina isipokuwa tu Wakuu wa Serikali za Washirika watakuwa ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa kuzingatia kuwa iwapo Rais wa Muungano anatoka upande mmoja wa Muungano, makamu wa kwanza atatoka upande wa pili wa Muungano. Makamu wa Rais wanaweza kukaimu Urais kwa masharti maalumu yatakayowekwa na Katiba.

Mapato na mgawanyo wa Mapato ya Muungano katika Serikali Tatu

Dola inapasa kuwa na rasilimali za kutosha na ziada inaweza kugawa kwa Washirika na Mikoa katika wajibu wa kuhakikisha maendeleo yanawiana. Dola pia inaweza kuwa na miradi ya Muungano. Kuna haja ya kuangalia kwa umakini mkubwa suala hili la mapato ya Serikali ya muungano kama kweli kuna nia ya dhati ya kuendelea kuwa na Muungano. Mapendekezo yangu ni kama ifuatavyo;

Mapato ya Muungano

1. Ushuru wa Forodha
2. Mrahaba wa uvunaji wa Rasilimali ambapo 25% itabaki kwenye mkoa wenye rasilimali na 75% itatumika na Serikali ya Muungano kugawa kwenye mikoa kwa mujibu wa ‘formulae’ itakayokubaliwa kwa kuzingatia idadi ya watu, kiwango cha umasikini na ukubwa wa kijiografia.
3. Ushuru wa Bidhaa na huduma ambapo 60% itagawiwa kwa nchi Washirika kwa ajili ya miradi maalumu ya muungano.
4. Mapato kutoka kwenye kampuni za kibiashara za Serikali ya Muungano na gawio la Benki Kuu ya Tanzania.

Mapato ya Serikali za Washirika

1. Kodi ya Mapato ya watu binafsi na Makampuni
2. Kodi ya Ongezeko la Thamani au kodi kama hiyo
3. Tozo mbalimbali zitakazotungwa kwa mujibu wa sheria
4. Mapato yasiyo ya kikodi kutoka idara na Wizara za Serikali.

Mapato ya Mikoa

1. 25% ya Mrahaba kutokana na uvunaji wa Rasilimali/maliasili inayopatikana katika mkoa husika
2. 10% ya makusanyo ya kodi ya mapato ya watu binafsi na makampuni kutoka katika mkoa husika
3. Mgawo kutoka Serikali ya Muungano
4. Mgawo kutoka Serikali ya Washirika
5. Tozo mbalimbali zitakazoanzishwa kwa mujibu wa sheria ndogo ndogo zitakazopitishwa na Mabaraza ya Mikoa

Zitto Kabwe ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini na pia Mjumbe wa BMK

RaiaTanzaniq


No comments:

Post a Comment