Sunday, January 26, 2014

HII KALI: AFISA ANASWA KWA RUSHWA YA KILO 12 ZA NYAMA

Afisa mifugo na mkaguzi wa nyama katika machinjio ya Mitunduruni, Manispaa ya Singida, Edwin Shangwel Mtae, ameburuzwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi mjini Singida kwa tuhuma ya kupokea rushwa ya nyama ya ng'ombe kilo 12 na nusu. 

Mapema mwendesha mashitaka mwanasheria wa TAKUKURU mkoa wa Singida, Dominic Maganga, alidai mbele ya Hakimu Joyce Minde, kuwa mnamo septemba 28 mwaka jana, mshitakiwa bila halali aliomba na kupokea rushwa ya nyama ya ng'ombe yenye uzito wa kilo 12 na nusu thamani yake ikiwa shilingi 62,500. 

Maganga alisema kitendo cha mtuhumiwa ni kinyume na kifungu cha 15 cha sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa no.11/2007. Akifafanua zaidi, alisema taarifa walizozipokea ofisini kwao ni kwamba mshitakiwa alikuwa amejenga tabia sugu ya kuomba rushwa ya nyama za mifugo hususani maini, figo na moyo toka kwa wafanyabiashara wa nyama wa Singida mjini. 

Alisema kuwa mfanyabiashara asiye kubaliana na ombi hilo la rushwa ya nyama, alinyimwa kibali cha kuuza nyama ya mifugo. 

"Mnamo septemba 28 mwaka jana majira ya asubuhi,mtuhumiwa alifanyiwa mtego wa rushwa na kukamatwa na maafisa wa TAKUKURU wa mkoa wa Singida,akiwa amepokea rushwa ya nyama kiasi cha kilo 12 na nusu",alisema. 

Bw. EdwinMtae amekanusha kutenda makosa hayo, na kesi yake inatarajiwa kutajwa tena februari sita mwaka huu. Afisa huyo wa mifugo alifanikiwa kutekeleza masharti ya dhamana ambayo ni kuwa na wadhamini wawili wa ahadi ya shilingi laki tano kila mmoja.


No comments:

Post a Comment