Wednesday, April 13, 2016

MACHINJIO VINGUNGUTI YAFUNGWA KWA UCHAFU


Gazeti la Majira

MAMLAKA ya Chakula na Dawa nchini (TFDA), imeyafunga machinjio ya Vingunguti, Dar es Salaam kwa muda usiojulikana kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ya uchafu wa mazingira na uchakavu wa miundombinu.

Machinjiao hayo yamefungwa jana baada ya Maofisa wa TFDA kufanya ukaguzi na kujiridhisha kuwa, mazingira yaliyopo katika machinjio hayo ni hatarishi, si salama kwa afya za wachinjaji, wafanyabiashara na walaji wa nyama.

Daktari Mkuu wa mifugo katika machinjio hayo, Hassan Mgwalu, alisema TFDA wamefikia uamuzi huo baada ya kujiridhisha na mambo 18 yanayohusiana na mazingira, afya za walaji, wachinjaji pamoja na ubovu wa miundombinu ikiwemo ya maji na vyoo.

Sababu nyingine ni uuzwaji nyama kuongezeka katika mazingira hatarishi, ongezeko la idadi ya watu, uchakavu wa ndoano za kutundikia nyama, uzio usio na ubora kiasi cha kuruhusu watu kuingia machinjioni kupitia maeneo yasiyo rasmi.

Pia TFDA ilidai ndani ya machinjio hayo kuna idadi kubwa ya mashimo ya kutupa nyama zisizofaa, damu kuchemshwa na kukaushwa ndani ya machinjio, idadi ndogo ya wakaguzi wa nyama ambayo haiwiani na wanyama wanaochinjwa.

Katibu wa Umoja wa Wafanyabiashara wa Machinjio hayo, Joel Meshack, alisema kufungwa kwa machinjio hayo ni pigo kubwa kwao kwani hawatafanya biashara, nyama itapungua sokoni na kuwaathili walaji, wafanyakazi katika machinjio hayo kukosa ajira.

Diwani wa Kata ya Vingunguti ambaye pia ni Naibu Meya wa Manispaa ya Ilala, Omary Kumbilamoto, alisema ufungwaji wa machinjio hayo utaathiri vipato vya watu wake.

"Sehemu kubwa ya wakazi wa Vingunguti maisha yao  machinjio haya, namuomba Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala atekeleza kwa haraka maelekezo ya TPDF ili machinjio yafunguliwe," alisema.

Naye Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala, Isaya Mgulumi, alisema tayari analishughulikia kwa karibu suala hilo, taratibu za manunuzi ambazo haziwezi kikiukwa kisheria zinaendelea, muda wowote kuanzia leo vifaa kwa ajili ya marekebisho ya machinjio hayo vitafikishwa eneo hilo.
"Kama TFDA wameona kasoro juu ya viwango vinavyohitajika kwa machinjio, ofisi yangu inafanya jitihada za makusudi kurekebisha kasoro, siwezi kujua lini tutakamilisha maagizo haya," alisema.

Aliwatuhumu wafanyabiashara katika machinjio hayo kwa kushindwa kufuata taratibu za uendeshaji machinjio, kuuza nyama hadi mchana jambo ambalo halikubaliki na kuahidi kuweka utaratibu mpya machinjio hayo yatakapofunguliwa.

Machinjio ya Vingunguti yenye wafanyabiashara zaidi ya 350 yana uwezo wa kuchinja ng'ombe 300, lakini baada ya wafanyabiashara kuongezeka kutokana na kufungwa kwa machinjio ya Kimara, ng'ombe kati ya 550 hadi 600 wanachinjwa kwa siku.




1 comment:

  1. afya ya jamii , public health ni ya muhimu kuangaliwa kwa kina na mapana

    ReplyDelete