Walimu wa Mkoa wa Dar es Salaam wanaidai Serikali jumla ya sh. Bilioni 1.1 za madai yao mbalimbali kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2013 hadi 2015.
Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Chama cha Walimu (CWT) Mkoa wa Dar es Salaam, Mwalimu Amina Kisenge (pichani kushoto), katika kikao cha baraza la dharura la chama hicho lililoketi hivi karibuni.
"Awali CWT ilikua ikidai jumla ya Sh.Bilioni 3.9 kabla ya kupunguza kiasi cha Sh.Bilioni 1.9 mapema mwaka huu.
Kwa mujibu wa Mwenyekiti, madeni hayo ni pamoja na malimbikizo ya nauli za likizo kuanzia mwezi Juni na Desemba, 2013 lakini pia Juni na Desemba mwaka jana.
Malimbikizo mengine ni pamoja na pesa ya kuwasafirisha wastaafu kwenda majumbani kwao," alisema Kisenge na kuongeza
"Uhamisho wa walimu kutoa kituo kimoja kwenda kingine ikiwa ni posho ya usumbufu na ya kujikimu pamoja na pesa za gharama za masomo baada ya walimu kujigharamia kujisomesha, imekuwa pia ni tatizo kwa serikali kutoa," alisema .
Aliongeza kwamba changamoto nyingine inayowakabili walimu ni mfuko wa PSPF kutowalipa walimu wastaafu kwa wakati ambapo walimu waliostaafu Januari hadi Septemba mwaka huu hawajalipwa mafao yao.
Alibainisha kuwa kero nyingine ni walimu kutopandishwa madaraja kwa wakati na kwa wale wanaobahatika kupanda madaraja, mishahara yao hairekebishwi.
Wakati huohuo, CWT iliitaka serikali ya awamu ya tano kuharakisha matumizi ya chombo cha ajira kwa walimu kilichopitishwa na serikali ya awamu ya nne kwamba chombo hicho ndicho mkombozi wao.
No comments:
Post a Comment