Friday, May 02, 2014

YANGA YAZIDI KUPATA PIGO, DOMOYO ASAINI MKATABA AZAM NA TFF

Mabingwa wa ligi kuu soka Tanzania Bara, Azam Fc ndani ya siku mbili wamefanya usajili wa wachezaji wawili kutoka klabu ya Yanga SC ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa mapendekezo ya kocha mkuu, Mcameroon, Joseph Marius Omog.

Mapema wiki hii walifanikiwa kumsainisha aliyekuwa mshambuliaji wa Yanga, Mrundi Didier Kavumbagu kwa mkataba wa mwaka mmoja, huku kipengele cha kuongezewa mwaka mwingine kikiwepo kulingana na uwezo atakaouonesha.

Wakati wapenzi wa soka wakijadiliana usajili wa Kavumbagu, juzi wengi walishituliwa na usajili mwingine mkubwa wa kiungo mahiri wa ukabaji wa Yanga, Frank Domayo `Chumvi”. Domayo alisaini Mkataba wa miaka miwili kuitumia klabu ya Azam, huku taarifa zikieleza kuwa mkataba wake na Yanga ulikuwa umemalizika mwishoni mwa msimu uliopita.

Usajili wa Domayo ulifanyika jana katika kambi ya timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars iliyopo Tukuyu jijini Mbeya kwa maandalizi ya mchezo wa kirafiki wa kimataifa dhidi ya Malawi mei 4 mwaka huu uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.


Stars ipo katika mipango ya mchezo huo na wachezaji wote wanaufikiria, lakini kwa Domayo imekuwa tofauti ambapo akiwa huko ameamua kusaini Azam fc. Ukirejea nyuma sio mara ya kwanza mchezaji kusaini akiwa katika kambi ya timu ya taifa ya Tanzania. Kelvin Yondani wakati anasaini Yanga kutokea Simba alikuwa kwenye kambi ya Taifa stars.

Ilielezwa kuwa alitoroshwa na kiungozi mmoja kwenda kusaini Yanga. Kitendo kile kilitafsiriwa kuwa utovu wa nidhamu, lakini baadaye suala hilo lilizimwa kiaina kwasababu ni utamaduni wetu.

Domayo si mara yake ya kwanza, kwasababu miaka miwili iliyopita wakati akijiunga na Yanga kutoka JKT Ruvu alisaini mkataba wake akiwa kambi ya Stars. Baada ya usajili huo kukamilika, Katibu wa Azam FC, Nassor Idrisa Mohamed ‘Father’ amekaririwa na tovuti ya Azam akisema katika kuendelea kukiimarisha kikosi chao kwa ajili ya msimu ujao wamepiga hatua nyingine kwa kumsaini Domayo.

“Kama unavyojua, baada ya kumaliza msimu vizuri tukiwa mabingwa wa Bara, tuligundua mapungufu kwenye kikosi chetu na kwa ushauri wa mwalimu wetu (Joseph Marius Omog) ndiyo tunayafanyia kazi,”alisema Father.

Domayo anakuwa mchezaji wa wa pili ndani ya siku mbili kusajiliwa na Azam FC kutoka mabingwa wa zamani na mabingwa wa kihistoria Tanzania Bara, Yanga SC baada ya jana klabu hiyo kumsaini mshambuliaji Mrundi Didier Kavumbangu.

Kufautai usajili wa aina hiyo kujitokeza tena katika kambi ya Taifa stars, shirikisho la soka Tanzania, TFF limeshituka na kuanza taratibu za kuchunguza suala hilo linaloihusisha Azam fc na mchezaji Frank Domayo akiwa kambini.

Taarifa iliyotumwa na afisa habari wa TFF, Boniface Wambura Mgoyo, asubuhi hii inasema kuwa: “Kutokana na tukio lililotokea jana (Aprili 30 mwaka huu) kwenye kambi ya timu ya Taifa (Taifa Stars) iliyopo Tukuyu mkoani Mbeya likihusisha usajili wa baadhi ya timu, Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi amemteua Wakili Wilson Ogunde kuchunguza mlolongo mzima wa tukio hilo.


Baada ya kukamilisha uchunguzi wake, Wakili Ogunde ataishauri TFF kuhusu hatua za kisheria na kikanuni za kuchukua. TFF inatoa wito kwa wachezaji, klabu na wadau wa mpira wa miguu kufuata kanuni na taratibu katika utendaji wao”.


No comments:

Post a Comment