Tuesday, May 20, 2014

BREAKING NEWS; MAJAMBAZI YAPORA PESA KAWE CLUB JIONI YA LEO

Mtu mmoja ambaye hakutaka kujulikana jina lake amekumbwa na mkasa wa kuvunjiwa na kuibiwa pesa kiasi kisichopungua shilingi za kitanzania milioni 10 alipokuwa katika mgahawa wa Kawe Club jijini Dar es Salaam leo jioni.

Akielezea tukio hilo, shuhuda ambaye pia hakutaka kutajwa jina lake anasema ilikuwa majira ya saa kumi na nusu wakati majambazi wasiopungua 5 walipovunja kioo upande wa kushoto mbele cha gari aina ya Toyota Hilux yenye usajili T163CUL (Pichani) na kuchukua hela kiasi cha shilingi milioni 10.

“Walikuja na pikipiki wakati mi naosha gari hiyo, nikiwa upande wa pili (yaani wa dereva) naosha tairi ya mbele, nikasikia mshindo wa kuvunjwa kioo, nikaona watu wawili kwenye pikipiki mmoja ameshika bunduki wakichukua pesa kwenye gari na kisha wakaondoka mbio” alieleza kijana huyo

 (Kushoto ni ganda la risasi kama lilivyokutwa eneo la tukio)

Kijana huyo anasema alipiga kelele za wezi, walinzi wakiwa wanashangaa hawajui la kufanya. Kwa mujibu wa kijana huyo, kelele zake zikasaidia kwani watu wanaofanya shughuli zao eneo la baharini karibu na Kawe Club walisikia na kuanza kuwakimbiza watu hao.

Walipofika mbele kidogo wakiwa wanawakaribia, ndio jambazi mmoja akapiga risasi hewani ndipo watu wote wakalala chini kuhofia usalama wao.

Kijana mwingine aliyekuwa anapita njia ya kuelekea Kawe Beach anasema aliposikia kelele ya risasi kisha akaona pikipiki gari aina ya RAV4 zikifuatana kwa mwendo mkali sana.

Imedaiwa tukio zima lilichukua si zaidi ya dakika tatu mpaka watu hao kutokomea. Hata hiyvo meneja wa Kawe Club alifanikiwa kuita polisi ambao walifika muda si mrefu kufuatilia tukio hilo.

Mmiliki wa gari hilo anasema alikuwa ametoka benki ya CRDB Mlimani City kuchukua pesa hizo na ndipo alipoamua kwenda kula samaki Kawe Club kabla ya kukumbwa na mkasa huo.



“Nikiwa ndani nikasikia alam ya gari inalia, lakini pia nilisikia makelele ya watu walidai mwizi mwizi, ndo kutoka nikakuta wameshatokomea. Wamefanikiwa kuchukua hela pekee lakini wameacha silaa yangu iliyokuwa katika droo ya gari, nafikiri hawakujua kama ipo lasivyo na yenyewe ingekwenda” alieleza mtu huyo


No comments:

Post a Comment