Wednesday, June 01, 2016

TATIZO LA HEWA YA UKAA KUPUNGUA HAPA NCHINI

Frank Mvungi-Maelezo

Wakala wa Taifa wa Utafiti wa Nyumba Bora na Vifaa vya Ujenzi (NHBRA) umeanza kufanya utafiti utakaosadia kupunguza kiwango cha Hewa ya Ukaa (green house gases) kinachozalishwa kutokana na shughuli za ujenzi ili kupunguza uharibifu wa mazingira.

Akizungumza na Waandishi wa Habari leo jijini Dar es salaam Mhandisi Heri Hatibu kutoka wakala huo amesema utafiti utasaidia kupunguza gharama za Ujenzi hapa nchini.

Akizungumzia Malengo ya Utafiti huo Hatibu amesema kuwa, utasaidia kupunguza kiwango cha nishati kinachotumiwa kwenye nyumba kwa ajili ya kupooza hewa hivyo kuokoa fedha inayoweza kutumika kufanya mambo mengine.

“Sekta ya Ujenzi inachangia asilimia 40 ya hewa ya ukaa hivyo lengo la utafiti huu ni kusaidia kuondoa tatizo hili mara baada ya utafiti wetu kukamilika.” Alisisitiza Mhandisi Hatibu.

Aidha Hatibu amesema kuwa, utafiti huo utawezesha kusanifu majengo yatakayotumia nishati kidogo kwenye hatua ya ujenzi na hata wakati wa matumizi ya majengo husika. Pia utachochea matumizi ya vifaa vya Ujenzi vinavyopatikana katika maeneo ya karibu na shughuli za ujenzi.

Pia utafiti huo utasaidi kutoa elimu kwa wadau wa ujenzi kuhusu nishati mbadala katika kutekeleza shughuli za ujenzi, ikiwemo kuacha kukata miti.

Vile vile wananchi wataelimishwa kuhusu njia bora za uchomaji wa matofali ili waweze kutumia vifaa vingine badala ya kukata miti kwa ajili ya uchomaji matofali.

Matokeo ya utafiti huo unaotarajiwa kukamilika kabla ya mwisho wa mwaka huu yatasaidia wadau wa sekta hii kupanga mipango ya ujenzi itakayosaidia kupunguza athari katika mazingira zinazosababishwa na matumizi makubwa katika uzalishaji vifaa vya ujenzi na hata katika ujenzi.Utafiti huo unafanyika katika Mikoa ya Dar es salaam, Dodoma, Morogoro na Tanga.





No comments:

Post a Comment