Monday, January 20, 2014

WAARABU NA WAKIMBIZI WAMEUA TEMBO 20 CHUNYA

Chunya 

Wakimbizi na jamii ya Waarabu kutokea mikoa ya Kigoma na Tabora wamedaiwa kuvamia pori la Akiba la Piti lililopo kata ya Mafyeko wilayani Chunya na kuua jumla ya tembo 20. 

Pori la Piti lipo mpakani mwa wilaya za Sikonge mkoani Tabora na Manyoni mkoani Singida.  Akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea wilayani humo mwishoni mwa wiki Kaimu Ofisa Wanyamapori wa wilaya ya Chunya Abdallah Mgonja alisema kuwa Tembo 13  waliuawa kwa kupigwa risasi na mizoga yao kutelekezwa porini. 

Alisema walibaini kutumika kwa wakimbizi katika ujangiri huo baada ya kuokota bunduki ya kivita aina ya SGM ambayo inatumika na wakimbizi wa nchi jirani ambao hutumiwa na waarabu kufanya ujangiri huo. 


Alisema katika operesheni hiyo ya 2012-’13 maofisa wanyamapori waliokota meno 6 ambapo majangiri walikimbia na kwamba asilimia kubwa ya majangiri wanaovamia eneo hilo ni wakimbizi wanaotumiwa na Waarabu wanatokea mikoa ya jirani ya Tabora na Kigoma.

Bw.Mgonja alisema kuwa eneo hilo la Pori la Akiba la Piti ambalo awali lilikuwa pori la wazi kabla ya kupandishwa daraja limekuwa likivamiwa mara kwa mara na majangiri ambao makao makuu yao yapo katika kata ya Kitunda, Sikonge na Mafyeko.  ‘’Mwishoni mwa mwaka jana tumekuta mizoga ya Tembo watatu,Twiga wawili waliouawa na kukatwa vichwa,

Nyati watano, Swala 6, pia tulikamata bunduki aina ya SMG inayotumiwa vitani, hawa wanategwa kwa nyaya na kuuawa kwa magobole’’alisema Bw. Mgonja.  Alisema kuwa hadi sasa kesi tatu zinazohusiana na ujangiri zimefikishwa mahakamani ambapo kati ya hizo kesi mbili  zinahusu Pembe za Ndovu. 

Bw. Mgonja alisema kuwa wilaya hiyo ina aina zote za wanyama wanaopatikana katika maeneo mengine ya hifadhi za Katavi na Ruaha isipokuwa wanyama aina ya Faru na Nyumbu. 

Wilaya ya Chunya ina jumla ya mapori ya akiba mawili ya Piti na Lukwati na pori la wazi la Rungwa ambalo lipo upande wa Chunya na sehemu ya Hifadhi ya Taifa ya Ruaha na kwamba kuna jumla ya vitalu 9 na makampuni 7 ambayo yanaendesha uwindaji wa kitalii.




No comments:

Post a Comment