Monday, July 08, 2013

SHULE ZAFUNGWA YOBE

Shule za umma za sekondari zimeamrishwa kufungwa katika jimbo la Yobe Kaskazini mwa Nigeria baada ya mauaji ya halaiki ambayo wapiganaji wa kiisilamu wanashukiwa kuwaua wanafunzi 22 na kuiteketeza shule yao.

Gavana wa Yobe, Ibrahim Gaidam amelaani mashambulizi hayo yaliyofanyika Jumamosi katika shule la Mamudo na kuyaita ya kinyama.


Nigeria imelaumu wapiganaji wa kiisilamu wa Boko Haram, waliolenga kushambulia shule mbili katika eneo hilo mwezi Juni .

Tafsiri ya jina Boko Haram, inamaanisha elimu ya kimagharibi imeharamishwa.

Mamia ya shule zimeteketezwa na wapiganaji wa kiisilamu tangu mwaka 2010.

Alipoitembelea shule hiyo Jumapili, bwana Gaidam aliwataja washambulizi kama watu wasioheshimu utu.

Aliamuru shule za umma kufungwa hadi mwanzo wa muhula mpya wa shule mwezi Septemba, ili kuruhusu serikali ya majimbo pamoja na maafisa wa serikali kuangalia njia za kuhakikisha usalama katika shule za umma.

Pia aliitaka serikali kuondoa marufuku iliyowekewa upeperushaji wa masafa ya simu za mkononi katika jimbo hilo.

Yobe ni moja ya majimbo ambako rais Goodluck Jonathan alitangaza sheria ya hali ya hatari mwezi Mei na kuwapeleka mamia ya majeshi katika eneo hilo.

Walioshuhudia tukio hilo walisema baadhi ya wathiriwa wa shambulizi waliteketezwa wakiwa hai katika shambulizi la Jumamosi wakati wengine wakipigwa risasi walipokuwa wanakimbilia usalama wao.

Wazazi walikuwa na wakati mgumu kutambua miili ya wanao iliyoteketezwa kiasi cha kutotambulika.

Walionusurika walisema kuwa watu wanaoshukiwa kuwa wapiganaji wa kiisilamu waliwasili katika shule hiyo wakiwa na mafuta ya petroli kwa wingi tayari kuiteketeza shule.

Wale waliojeruhiwa kwenye shambulizi hilo walipokea matibabu ya bure.

HABARI  HII NI KWA HISANI YA SHIRIKA LA HABARI LA UINGEREZA IDHAA YA KISWAHILI BBC

No comments:

Post a Comment