Friday, July 22, 2016

MWENYEKITI CCM MARA ATUHUMIWA KWA USALITI

Na Mwandishi Wetu, MWANZA

BAADHI ya wenyeviti wa Kata,Matawi pamoja na mabalozi wa nyumba kumi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) katika Wilaya za Mkoa wa Mara wamemtuhumu Mwenyekiti wa chama hicho mkoani humo Christopher Sanya kuwa alikihujumu kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka jana na kusababisha kipoteze majimbo manne kati ya tisa na kumtaka ajiuluzu kabla ya kutimuliwa.

Pia walidai kuwa anaongoza kwa majungu akiongozwa na mmoja wa wabunge wa majimbo ya mkoa wa Mara huku wakimtuhumu kujihusisha na kundi linalopinga Rais John Magufuli asikabidhiwe Uenyekiti wa CCM Taifa na amekuwa akiwashawishi wajumbe wasimpigie kura.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili jijini Mwanza jana kwa sharti la hifadhi ya majina wenyeviti hao kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka jana alikisaliti chama pamoja na kuwachonganisha wanachama na kusababisha majimbo manne kunyakuliwa na wagombea wa UKAWA.

Walieleza kuwa Sanya kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka jana alitafuna posho za mabalozi wa CCM akishirikiana na Katibu msaidizi wa CCM wakashindwa kufanya kampeni kisha katibu huyo akahamishiwa wilayani Rorya.

Kutokana na tuhuma hizo wanachama wa Wilaya za Rorya,Serengeti, Tarime na Bunda wamemwomba mwenyekiti mpya wa CCM Taifa atakapobidhiwa rungu atumbue jipu hilo linalokwamisha maendeleo ya chama na wananchi.

“ Tunafahamu mwenyekiti wetu wa CCM mkoa wa Mara ni jipu na msaliti mkubwa kwenye kampeni alishiriki kuwaangusha wagombea wetu Bunda (Wassira) na Serengeti (Kebwe) kwa kuwasaidia wapinzani.Matokeo baada ya kutangazwa alifanya sherehe” alisema mmoja wa wenyeviti hao wa matawi na kata kwa sharti la hifadhi ya jina.

Wenyeviti hao walionya kuwa endapo mwenyekiti mpya akipuuuza kumfukuza kwenye chama kwa usaliti pamoja na washirika wake basi CCM Mara itaparaganyika kama si kufutika na majimbo yaliyopotea hayatarudi na hata waliyoshinda watayapoteza.

Naye Sanya akizungumza kwa simu na gazeti hili kuhusiana na tuhuma hizo alikana na kumtuhumu Mwenyekiti wa CCM wa Wilaya ya Rorya Samwel Kiboye “ Namba 3” kuwa ndiye anatengeza habari hizo kwani hakuna mwenyekiti anayeweza kumtuhumu.

“ Usipoteze muda kwa mambo kama hayo,kama ni malalamiko tuna vikao vya kuyasikiliza na kutoa uamuzi,uchaguzi ulishaisha na wananchi walifanya uamuzi.Tuhuma za usaliti sina sera hiyo ya kuhujumu chama na ukweli utabaki pale pale.Mi ni Mwenyekiti, acha mambo hayo usipoteze muda,

“ Wananchi na wanachama si wajinga.Tatizo la kupoteza majimbo linafahamika maana baada ya uchaguzi tulikaa na kubaini nani alifanya nini,hivyo hakuna logic.Lakini kuna wakati tuliwaudhi wananchi na jimbo moja hilo la Bunda haliwezi kuwa na madhara kiasi hicho,” alisema Sanya.

Mwenyekiti huyo alidai kuwa yote hayo yanatengezwa na Mwenyekiti wa CCM wa Wilaya moja kwa sababu anataka kugombea na hivyo anatafuta nafasi ya kumchafua na kuelea kuwa binafsi anaishi vizuri na wenyeviti wake wa wilaya na watashangaa kusikia mambo hayo.

“Uchaguzi wa kiti ujao ndio umeanza hivyo,wana CCM sio wajinga, niko imara na chama changu na fitna ni sehemu ya siasa.Namba 3 ndiye anatengeneza story ili apate kunichafua sababu anataka kugombea uenyekiti na mimi lazima nitulize hali hiyo maana uchaguzi bado, muda ukifika wanachama wataamua nani anafaa kuwaongoza,”alisema Saa
nya kwa simu.

No comments:

Post a Comment