Saturday, December 28, 2013

POMBE YAMUUA MFANYAKAZI WA TIGO

Shinyanga 

Katika hali isiyokuwa ya kawaida mfanyakazi mmoja wa kampuni ya simu za mkononi ya TIGO mkoani Shinyanga amekufa papo hapo baada ya kudaiwa kunywa pombe nyingi aina ya Konyangi kupita kiasi. 

Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo wamemtaja mfanyakazi huyo kuwa ni Godi Mangala (34) aliyekuwa akiishi mtaa wa Majengo mapya kata ya Ngokolo manispaa ya Shinyanga ambalo limetokea juzi saa moja usiku wakati wa sikukuu ya krismasi. 


Mashuhuda hao wamewaeleza waandishi wa habari mjini kwamba siku hiyo ya tukio, Godi akiwa na marafiki zake katika moja ya glosari za mjini humo waliamua kupata vinywaji ambapo waliamua kunywa pombe hiyo kwa kushindana ili kuweza kumpata bingwa wa utumiaji wa kilevi hicho.

Walisema muda mfupi baada ya marehemu kuonesha ubingwa wake katika unywaji wa pombe hiyo alionesha dalili za kuzidiwa na kuishiwa nguvu hali ambayo ilisababisha rafiki zake wamtafutie usafiri na kumrudisha nyumbani kwake ili apumzike. 

“Hata hivyo tulipoona hali yake inaendelea kuwa mbaya tulichukua uamuzi wa kumkimbiza katika hospitali ya serikali mkoani Shinyanga ili aweze kupatiwa matibabu haraka lakini hata hivyo alifariki dunia kabla ya kufikishwa hospitali,” alieleza mmoja wa marafiki wa marehemu ambaye hata hivyo hakupenda kutajwa jina gazetini. 

Kwa upande wake John Maganya ambaye pia ni mmoja wa marafiki wa marehemu alielezea kushitushwa kwake na tukio hilo ambalo limesababisha kifo cha rafiki yake ambaye hata hivyo alisema enzi za uhai alikuwa ni mzoefu katika unywaji wa pombe japokuwa kuna wakati alikuwa akizimia na kuzinduka. 

“Nimeshitushwa na kifo cha rafiki yangu, kwani kama ni pombe mbona alikuwa mzoefu, nafikiri hii Konyagi aliyokuwa anakunywa na wenzake imesababisha kifo chake, maana tumeelezwa kwamba alikunywa mizinga mitano kwa mkupuo, ni hatari,” alieleza Maganya. 

Kwa upande wake mganga mfawidhi katika hospitali ya serikali mkoani Shinyanga, Dkt. Fredrick Mlekwa alikiri kupokea mwili wa marehemu huyo juzi mnamo saa moja usiku na kwamba baada ya kuchunguzwa na kubainika tayari ameishafariki alielekeza mwili huo ukahifadhiwe katika chumba cha kuhifadhia maiti hospitalini hapo. 

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga, Evarist Mangala alisema hakuwa na taarifa juu ya tukio hilo na kwamba huenda ndugu wa marehemu hawakuona umuhimu wa kutoa taarifa polisi ya kifo cha ndugu yao. 


Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana jana mjini hapa, tayari ndugu wa marehemu waliuchukua mwili wake na kupelekwa jijini Mwanza eneo la Mabatini ambako ulitarajiwa kuzikwa leo mchana (Jumamosi). 


No comments:

Post a Comment