Sunday, January 17, 2016

SERIKALI YALIFUTA GAZETI LA MAWIO


Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeamua kulifuta kutoka katika Daftari la Usajili wa Magazeti, gazeti la “MAWIO”. Amri ya kulifuta gazeti hilo imetolewa kwa Tangazo la Serikali Na. 55 lililotolewa tarehe 15 Januari, 2016.

Tetesi za kufingiwa kwa gazeti la Mawio(Pichani Kushoto) zilianza kuzagaa jana katika mitandao ya jamii hususani ule wa Whatsapp, huku kukiwa na madai kuwa wahariri wa gazeti hilo kusakwa na polisi kutoka ofisi ya Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam.

Aitha taarifa hiyo iliyoshika kasi jana ilionesha kuwa polisi walifika katika ofisi za Mwanahalisi amber ni wachapishaji wa gazeti la Mawio mara kadhaa wakimtafuta Wahariri, Jabir Idrisa na Simon Mkina huku kukiwa na agizo lililotolewa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Mnauye katika Gazeti la Serikali(Pichani Kulia).

Uamuzi huo umetolewa kwa mujibu wa Sheria ya Magazeti Sura ya 229, kifungu 25(1). Hatua hii pia inazuia gazeti la Mawio kuchapishwa katika njia nyingine yoyote ikiwa ni pamoja na mitandao (Online publication) kwa mujibu wa Sheria ya Mawasiliano ya Kieletroniki na Posta Sura ya 306.

Serikali kwa masikitiko makubwa, imechukua uamuzi huu kutokana na mwenendo wa uandishi wa gazeti hilo usioridhisha wa kuandika na kuchapisha habari zenye mwelekeo wa uchochezi na kuhatarisha amani, utulivu na usalama wa nchi yetu.

Aidha, hatua hii ya kulifuta gazeti hilo imechukuliwa baada ya Msajili wa Magazeti kufanya juhudi kubwa za muda mrefu kuanzia Juni, 2013 hadi Januari, 2016 kumtaka Mhariri wa gazeti hilo kubadili aina ya uandishi wa habari na makala katika gazeti lake, bila mafanikio.


No comments:

Post a Comment