Friday, February 07, 2014

KENYATA ATAMANI KUKWEPA CHAKULA CHA MISAADA

Rais Kenyatta akizindua msafara wa lori zilizobeba chakula cha msaada kwa waathiriwa wa njaa
Maelfu ya watu wanaokabiliwa na uhaba wa chakula nchini Kenya wanatarajiwa kupata afueni baada ya Rais Uhuru Kenyatta kuzindua rasmi mpango wa kuwapelekea chakula cha msaada.

Lori kumi na moja ziliondoka Ikulu ya Rais mjini Nairobi zikiwa zimebeba maelfu ya tani za chakuka ikiwemo Mchele, Maharagwe na nafaka zingine ambazo watu wanaokabiliwa na njaa katika sehemu mbali mbali za nchi watafaidika navyo.

Kenyatta alikiri kuwa ni aibu kubwa kuwa nchi hiyo inatoa msaada wa chakula kwa raia wake ishara kuwa hapakuwa na mipango yoyote kuweza kuzuia hali hii.Hatua ya Rais Kenyatta inakuja wiki moja baada ya halmashauri ya kitaifa ya kupambana na ukame kuonya serikali kuhusu tisho la uhaba wa chakula ikisema kuwa majimbo 11 yenye zaidi ya watu milioni moja yanakabiliwa na tisho hilo la uhaba wa chakula.

Hata hivyo amesema kuwa serikali haina budi ila kufanya hivyo.

Ameelezea kuhusu mipango tofauti ya serikali inayonuia kukabiliana na tatizo la uhaba wa chakula ikiwemo kuanzisha miradi ya kukuza chakula, miradi ya unyunyiziaji mimea maji na miradi mingine kuhakikisha kuwa Kenya ina uwezo wa kutosha kujilisha.

Maeneo yanayokabiliwa na tisho la njaa ni pamoja na Samburu, Turkana, Garissa, Mandera, Wajir, Isiolo, Marsabit, Pokot, Baringo, Tana River jimbo na maeneo ya Lamu .

Waziri wa ugatuzi Ann Waiguru amesema kuwa chakula kingine cha msaada kinatarajiwa kupelekewa waathiriwa katika wiki chache zijazo.

Rais Kenyatta amesisitiza kuwa chakula kitaendelea kupelekwa hadi pale hali itakapokuwa sawa akisema kuwa mamilioni ya dola imetengwa kuhakikisha kuwa watu wanaokabiliwa na njaa wanapokea msaada.(BBC)


No comments:

Post a Comment