Thursday, June 23, 2016

WAKALA WA MAJENGO (TBA) YAKUSANYA BIL. 2.6

 Na Maelezo

Wakala wa Majengo nchini (TBA) wamefanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 2.6 sawa na asilimia 43 kwa kipindi cha miezi mitatu ambayo wapangaji wa nyumba hizo kushindwa kumalizia madeni wanayodaiwa

PICHANI: 
Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Majengo nchini (TBA) Bw. Elius Mwakalinga wa kwanza kushoto akiwaongoza wafanyakazi wa mamlaka hiyo kufanya usafi jijini Dar es salaam katika kuadhimisha kilele cha wiki ya utumishi wa Umma.

Akizungumza hayo katika kilele cha kuadhimisha wiki ya Utumishi wa Umma nchini Mkurugenzi Mtendaji wa TBA Bw. Elius Mwakalinga amesema kuwa wamefanikiwa kukusanya kiasi hiko cha fedha kutoka kwa wateja wao waliowapangisha majengo na bado wanaendelea kukusanya mpaka watakapomaliza.

“Kutokana na mkakati wa kukusanya mapato na kutoa huduma bora kwa wateja wetu tumefanikiwa kukusanya shilingi bilioni 2.6 katika kipindi cha miezi mitatu tuliyowapa wateja wetu kuweza kukamilisha malipo hayo” alisema Bw. Mwakilinga

Mbali na hayo Bw. Mwakilinga amesema kuwa wameamua kutumia siku hiyo kufanya usafi kwenye makazi ya watumishi wa umma na wakazi wengine ili kuweka mazingira bora kwenye miradi yao na jamii nzima kwa ujumla.
“Siku ya leo tumeamua kuitumia kufanya usafi kwenye maeneo ambayo tumeweka miradi yetu kwa watumishi wa umma pamoja na mazingira mengine ili kuepuka na magonjwa yasababishwayo na uchafu” alisisitiza Bw. Mwakilinga.

Aidha Bw. Mwakilinga amesema wanampango wa kupanua wigo wa huduma yao kwa kuwapangisha watumishi wa umma ambao wanastaafu waendelee kukaa kwenye nyumba hizo ili wasipate shida mara baada ya kustaafu.

Mbali na hayo Mkurugenzi Mtendaji huyo amesisistiza kuwa wataendelea na utaratibu wao wa kukusanya kodi na kuchukua nyumba zao kwa wale ambao wamekaidi amri yao ya kutolipia kodi nyumba hizo ili wapewe wengine ambao wana huitaji .

Wiki ya utumishi wa Umma imeadhimshwa kwa kila taasisi ya kiserikali kusikiliza na kutatua kero zinazowapata wateja wanaoutumia huduma za taasisi husika ili kuipeleka nchi katika utendaji bora na mafanikio kwa ujumla.

Wafanyakazi wa Wakala wa Majengo nchini (TBA) wakishiriki katika kufanya usafi jijini Dar es salaam ili kuadhimisha kilele cha wiki ya utumishi wa Umma.

Picha na Ally Daud-Maelezo



No comments:

Post a Comment